Ruka hadi kwenye maudhui makuu

Shinikizo la damu (Hypertension)


Utangulizi

Unaweza kuwa na shinikizo la damu (presha) kwa muda mrefu bila kuwa na dalili zozote. Muda wote huu ingawa unakuwa hauna dalili, uwepo wa shinikizo la damu huendelea kuathiri mishipa ya damu na kusababisha madhara makubwa mwilini kama vile magonjwa ya moyo na kiharusi.  Hivyo ni vizuri kujipima mara kwa mara ili kuepuka kuchelewa.   




Shinikizo la damu hutokea taratibu kwa kadri umri unavyozidi kuongezeka, hivyo kuathiri karibu kila mtu anapofikia umri mkubwa. Upimaji wake ni rahisi kwa hiyo ni vema ukapima ili kuweza kupambana na ugonjwa huu kwa msaada wa daktari.


Dalili

Watu wengi wana shinikizo la damu bila kujua au kuwa na dalili. Ni wachahe wanaweza kuwa na dalili kama vile kuumwa kichwa,kutokwa na damu puani na kupata shida ya kupumua. Dalili hizi si maalumu (spesific) na mara nyingi hazitokei mpaka shinikizo linapokuwa katika kiwango kinachohatarisha maisha.


Shinikizo la damu hutokea kwa namna mbili;

Kwanza: Hutokea bila uwepo wa ugonjwa sababishi. Hii ni kwa sababu tu ya mishipa kupoteza uwezo wake wa kutanuka kutokana na umri.

Pili: Hutokea panapokuwa na ugonjwa sababishi kama vile;
·         Ugonjwa wa figo
·         Kansa ya tezi iliyo juu ya figo
·         Magonjwa ya kuzaliwa ya mishipa
·         Unene kupindukia
·         Matumizi ya dawa kama vile dawa za maumivu,dawa za mafua,dawa za uzazi wa mpango n.k
·         Matumizi ya dawa za kulevya kama vile kokeini na amfetamini.


Sababu

·         Umri. Wanaume wana uwezekano mkubwa wa kupata shinikizo la damu mapema zaidi ya wanawake. ( wanaume chini ya miaka 64, wanawake baada ya miaka 65). Lakini ni vema kujua kuwa unaweza kupata ugonjwa huu katika umri wowote

·         Historia ya familia. Presha ni miongoni mwa magonjwa ya kurithi.

·         Matumizi ya tumbaku. Kemikali zilizopo kwenye tumbaku huharibu kuta za mishipa ya damu. Kuta zlizoharibika hazina uwezo wa kutanuka vizuri hivyo husababisha mtiririko wa damu kuwa mgumu.

·         Chumvi. Madini ya sodiam katika chumvi huvuta maji ndani ya mishipa ya damu na kusababisha shinikizo.

·         Unene wa kupindukia. Kadiri unavyozidi kuwa mnene ndivyo mfumo wa damu unavyozidi kuhitaji damu nyingi ili kulisha sehemu zote za mwili. Damu nyingi husababisha shinikizo.

·         Kuishi kwa kukaa bila mazoezi. Maisha ya kukaa bila kufanya mazoezi au kufanya kazi inayoongeza mapigo ya moyo yanachangia kupata presha.

·       Msongo wa mawazo. Msongo wa mawazo husababisha kutolewa kwa homoni ya kotizoni inayochangia kupandisha presha na kiwango cha sukari mwilini.

·         Uwepo wa magonjwa sugu kama vile figo, kisukari, unene n.k.


Madhara ya Shinikizo la Damu

Shinikizo la damu katika mishipa ya damu husababisha  kuharibika kwa viungo mbalimbali vya mwili.
Uharibifu huu huenda sambamba na kadiri presha inavyozidi kuwa ya juu na isipotibiwa kwa kuda mrefu.

Madhara yake ni kama ifuatavyo;
  •  Kiharusi au mshtuko wa moyo 
  •  Kupasuka kwa mishipa ya damu 
  •  Mtindio wa ubongo
  •  Kisukari
  •  Kupoteza kumbukumbu n.k.

Upimaji wa shinikizo la damu

Vipimo vya shinikizo la damu kitaalamu vimegawanywa katika sehemu nne;
  1. Kipimo cha kawaida ambacho ni chini au sawa na 120 mm za mekyuri kwa kipimo cha juu na chini au sawa na 80 mm za mekyuri kwa kipimo cha chini, kwa kifupi huandikwa 120/80mmHg
  2. Kupanda kwa mgandamızo wa damu: 120-129/80 mmHg
  3. Shinikizo la damu hatua ya kwanza:  130-139/80-89 mmHg
  4. Shinikizo la damu hatua ya pili: 140 au zaidi/90 au zaidi mmHg
Ikumbukwe kuwa upimaji huu lazima ufanywe mara tatu au zaidi kwa nyakati tofauti ili kupata matokeo sahihi. Wakati mwingine daktari hushauri ufuatiliaji wa kipimo cha shinikizo la damu kwa masaa 24 ili kujua mwenendo na visababishi kwa dhumuni la kuanzisha tiba sahihi ikiwemo kubadilisha jinsi mtu anavyoishi au dawa. 


Tiba

Mara nyingi shinikizo la damu katika hatua za mwanzo huanza kutibiwa kwa kubadilisha mwenendo wa maisha ya mgonjwa kama vile;

  • Kula chakula chenye mlo kamili na kupunguka matumizi ya chumvi,
  • Kufanya mazoezi ili kuimarisha mishipa pamoja na moyo,
  • Kupunguza uzito ,
  • Kupunguza au kuacha kunywa pombe na kuvuta sigara.
Hizo ni miongoni mwa hatua chache ambazo mgonjwa au hata mtu mwenye afya anaweza kuzichukua ili kuzuia kupata shinikizo la damu pamoja na madhara yake.

Endapo ugonjwa huu utashindikana kudhibitiwa kwa njia hizi basi daktari anaweza kukuanzishia dawa. Lakini kumbuka kinga ni bora kuliko tiba. 











               


Maoni

  1. Hili moja ya machapisho muhimu sana katika kuelimisha jamii!
    Chapisho limetoa mwongozo sahihi juu ya maradhi ambayo kwa asilimia kubwa huwakumba jamii yetu. Ni somo zuri sana nimelipenda kiukweli.

    JibuFuta

Chapisha Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Msongo wa Mawazo (Depression)

Msongo wa mawazo ni nini? Msongo wa mawazo  ( Depression ) ni mfadhaiko wa akili anaoupata mtu kutokana na shida, taabu, dhiki, matatizo au changamoto zinazomkabili katika maisha ya kila siku. Msongo wa mawazo hutokana na pale mtu anaposhindwa kukabiliana na jambo linalomtatiza. Msongo wa mawazo huwapata watu wa rika na asili zote. Tafiti zinaonyesha kuwa wanawake  hupata msongo wa  mawazo zaidi kuliko wanaume. Msongo wa mawazo ni tatizo la kimwili pamoja na kiakili. Dalili. kujisikia maumivu sehemu mbalimbali za mwili hasa kichwa, kukosa hamu ya kula au kula chakula kupitiliza,hasa vyakula vyenye madhara, kukosa hamu ya tendo la ndoa, kuwa na huzuni wakati wote na kujisikia mnyonge, kusahau kirahisi au kupungua kwa uwezo wa kufikiria, kujisikia mpweke au kukosa matumaini ya maisha, kupungua kwa uwezo wa kimasomo kwa wanafunzi, kuwa na hofu au kutokujiamini, kupungua au kuongezeka uzito bila kupenda, kushindwa kulala au kulala kupindukia, kukosa utulivu wa nafsi, kuba

Homa ya Findofindo (Tonsillitis)

Utangulizi   Findofindo ( Tonsillitis) ni nini?  Mafindofindo ni mashambulizi ya virusi au bakteria kwenye tezi za koo zijulikanazo kama findo. Asilimia 15 mpaka 30 ya mashambulizi haya yanatokana na bakteria ila asilimia kubwa hutokana na virusi.  Dalili za mafindofindo   Kwa kawaida ni ngumu kutofautisha kati ya maambukizi yatokanayo na bakteria na yale ya virusi ila leo nitakujuza siri ndogo. Zipo dalili za pamoja na zile za tofauti.  Zifuatazo ni dalili za pamoja za mafindofindo unazoweza kuzipata kwa wagonjwa waliopata maambukizi ya bakteria na yale virusi  Maumivu ya koo Kupata shida katika kumeza  Homa kali ( Zaidi ya nyuzi joto 38 za sentigredi)  Maumivu ya kichwa  Maumivu ya sikio  Utando katika findo Dalili zifuatazo zinaasilimia kubwa sana kupatikana kwa mtu mwenye mashambulio yatokanayo na virusi.  Homa ( zaidi ya nyuzi joto 38 za sentigredi)   Uvimbe shingoni ( upande mmoja au pande mbili)   Maumivu ya kichwa  Kutokwa na kamasi  Kutokwa na machozi   Kumeza kwa shida  Maum